Zambezi (mto)
| Mto wa Zambezi | |
|---|---|
| | |
| Chanzo | karibu na Mwinilunga, Zambia |
| Mdomo | Bahari ya Hindi |
| Nchi za beseni ya mto | Zambia, Kongo, Angola, Namibia, Botswana, Zimbabwe, Msumbiji |
| Urefu | km 2,574 |
| Kimo cha chanzo | m 1,500 |
| Kiasi cha maji kinachotolewa mdomoni | m³/s 7,000 |
| Eneo la beseni (km²) | km² 1,570,000 |
Zambezi (pia huandikwa Zambeze au Zambesi) ni mto wa nne kwa urefu barani Afrika, mto mrefu zaidi unaotiririka kuelekea mashariki barani Afrika, na mto mkubwa zaidi unaomwaga maji yake katika Bahari ya Hindi kutokea Afrika. Bonde lake la uondoaji maji linafikia eneo la kilomita za mraba 1,390,000 (maili za mraba 540,000),[1][2] ikiwa ni chini kidogo ya nusu ya bonde la Mto Nile. Mto huo wenye urefu wa kilomita 2,574 (maili 1,599) unaanzia nchini Zambia na kutiririka kupitia mashariki mwa Angola, kando ya mpaka wa kaskazini-mashariki wa Namibia na mpaka wa kaskazini wa Botswana, kisha kando ya mpaka kati ya Zambia na Zimbabwe hadi Msumbiji, ambapo unavuka nchi hiyo na kuishia katika Bahari ya Hindi.[3][4] Kivutio maarufu zaidi cha Mto Zambezi ni Maporomoko ya maji ya Victoria. Maporomoko yake mengine ni pamoja na Maporomoko ya Chavuma[5] na Maporomoko ya Ngonye.[6]
Beseni lake lina km² 1,570,000 au nusu ya mto Nile. Chanzo chake kiko Zambia, halafu mto unapita Angola mpakani na Namibia, Botswana, Zambia na Zimbabwe kwenda Msumbiji inapofikia Bahari Hindi katika delta ya km² 880.
Kwenye mwendo wa Zambezi pana maporomoko kadhaa hasa maporomoko ya Victoria Falls. Mengine ni maporomoko ya Chavuma mpakani mwa Zambia na Angola, halafu Ngonye Falls karibu na Sioma, Zambia ya magharibi.
Vyanzo vikuu viwili vya nishati ya umeme wa maji kwenye mto huo ni Bwawa la Kariba, ambalo linatoa umeme nchini Zambia na Zimbabwe, na Bwawa la Cahora Bassa nchini Msumbiji, ambalo linatoa umeme nchini Msumbiji na Afrika Kusini. Aidha, vituo vingine viwili vidogo vya kufua umeme nchini Zambia viko kwenye Maporomoko ya Victoria na Zengamina.[7]
Vyanzo
[hariri | hariri chanzo]Asili
[hariri | hariri chanzo]
Mto huo unaanzia kwenye dambo (ardhi chepechepe) nyeusi yenye kinamasi katika misitu minene ya miombo inayoinuka na kushuka, kilomita 50 (maili 31) kaskazini mwa Mwinilunga na kilomita 20 (maili 12) kusini mwa Ikelenge katika Wilaya ya Ikelenge mkoani Kaskazini-Magharibi, Zambia, ukiwa katika mwinuko wa takriban mita 1,524 (futi 5,000) juu ya usawa wa bahari.[8] Eneo linalozunguka chanzo hicho ni mnara wa kitaifa, hifadhi ya msitu, na eneo muhimu kwa ndege.[9]
Kuelekea upande wa mashariki mwa chanzo hicho, kigawaneo cha maji kati ya Mabonde ya Congo na Zambezi ni ukanda uliojitokeza wazi wa ardhi ya juu,unaotiririka takriban kutoka mashariki hadi magharibi na kushuka kwa ghafla upande wa kaskazini na kusini. Ukanda huu unakata na kutenganisha wazi bonde la Lualaba (tawi kuu la juu la Mto Congo) na lile la Zambezi. Katika maeneo ya jirani na chanzo hicho, kigawaneo cha maji hakijajipambanua kwa uwazi sana, lakini mifumo hii miwili ya mito haiungani.
Eneo linalopitisha maji kutoka Mto Zambezi ni uwanda wa juu mpana wenye kingo zilizomomonyoka wenye mwinuko wa mita 900–1,200 (futi 3,000–3,900), ambao kwa upande wa ndani kabisa umeundwa na matabaka ya miamba geu na kuzungukwa na miamba ya moto katika Maporomoko ya Victoria. Kule Chupanga, upande wa chini wa Mto Zambezi, matabaka membamba ya miamba ya mchanga ya rangi ya kijivu na njano, kukiwa na miviringo ya hapa na pale ya miamba ya chokaa, yanajitokeza juu kwenye sakafu ya mto wakati wa kiangazi, na haya yanaendelea hadi ng'ambo ya Tete, ambapo yanaambatana na mishipa mikubwa ya makaa ya mawe. Makaa ya mawe pia yanapatikana katika wilaya iliyo chini kidogo ya Maporomoko ya Victoria. Miamba yenye madini ya dhahabu inajitokeza katika maeneo kadhaa.
Zambezi ya Juu
[hariri | hariri chanzo]
Mto huo hutiririka kuelekea kusini-magharibi kuingia Angola kwa takriban kilomita 240 (maili 150), kisha unaungana na vijito vikubwa vya mto kama vile Luena na Chifumage vinavyotiririka kutoka nyanda za juu za upande wa kaskazini-magharibi. Unageuka kuelekea kusini na kutengeneza uwanda wa mafuriko, wenye mabadiliko makubwa sana ya upana kati ya majira ya kiangazi na masika. Unaingia kwenye msitu mnene wa kijani kibichi wa kiangazi wa Cryptosepalum, ingawa kwa upande wake wa magharibi, maeneo ya nyasi ya Zambezi ya Magharibi pia yanapatikana. Unapoingia tena nchini Zambia, unakuwa na upana wa karibu mita 400 (futi 1,300) wakati wa majira ya masika na utiririka kwa kasi kubwa, ukiwa na maporomoko madogo ya maji yanayoishia kwenye Maporomoko ya Chavuma, ambapo mto huo unapita kwenye ufa wa miamba. Mto huo unashuka kwa mita 400 (futi 1,300) katika mwinuko wake kutoka chanzo chake kilichopo mita 1,500 (futi 4,900) hadi kufika Maporomoko ya Chavuma yaliyopo mita 1,100 (futi 3,600), katika umbali wa takriban kilomita 400 (maili 250). Kuanzia eneo hili hadi Maporomoko ya Victoria, usawa wa beseni la mto ni tambarare sana, ukishuka kwa mita nyingine 180 (futi 590) pekee katika umbali wa karibu kilomita 800 (maili 500).[10]
Kijito chake kikubwa cha kwanza kuingia Zambezi ni Mto Kabompo uliopo mkoani Kaskazini-Magharibi nchini Zambia. Eneo la savana (nyika) ambalo mto huo unapita linabadilika na kuwa uwanda mpana wa mafuriko, ukiwa umetawanyika mitende ya Borassus. Upande wa kusini kidogo kuna makutano ya mto na Mto Lungwebungu. Hapa ndipo mwanzo wa Uwanda wa Mafuriko wa Barotse, ambao ni kivutio maarufu zaidi cha upande wa juu wa Zambezi, ingawa sehemu hii ya kaskazini haifuriki sana na inajumuisha visiwa vya ardhi ya juu vilivyopo katikati.[11]
Takriban kilomita 30 chini ya makutano ya Mto Lungwebungu, nchi inakuwa tambarare sana, na ule mwonekano wa asili wa Uwanda wa Mafuriko wa Barotse unajifunua, huku mafuriko yakifikia upana wa kilomita 25 wakati wa masika. Kwa zaidi ya kilomita 200 kuelekea chini ya mto, mzunguko wa kila mwaka wa mafuriko unatawala mazingira ya asili pamoja na maisha ya mwanadamu, jamii, na utamaduni. Takriban kilomita 80 mbele zaidi kuelekea chini, Mto Luanginga, ambao pamoja na matawi yake unanyonya maji katika eneo kubwa la upande wa magharibi, unaungana na Zambezi. Umbali mfupi tu kuelekea juu upande wa mashariki, mkondo mkuu unaungana wakati wa masika na maji yanayofurika kutoka mfumo wa Luampa/Luena.
Umbali mfupi kuelekea chini ya mto kutoka makutano ya Mto Luanginga ni Lealui, mji mkuu mmojawapo wa Walozi, wanaoishi katika ukanda wa Barotseland mkoani Magharibi nchini Zambia. Chifu wa Walozi anamiliki moja ya makazi yake mawili huko Lealui; lingine liko Limulunga, ambalo lipo kwenye ardhi ya juu na hutumika kama mji mkuu wakati wa majira ya masika. Kuhama kwa kila mwaka kutoka Lealui kwenda Limulunga ni tukio kubwa, linalosherehekewa kama moja ya sherehe za kitamaduni zinazojulikana zaidi nchini Zambia, yaani Kuomboka.
Baada ya Lealui, mto huo hugeuka kuelekea kusini-kusini-mashariki. Kutokea upande wa mashariki, unaendelea kupokea mito mingi midogo, lakini kwa upande wa magharibi, hauna matawi makubwa ya mto kwa umbali wa kilomita 240. Kabla ya hapo, Maporomoko ya Ngonye na maporomoko madogo ya maji yanayofuata yanazuia usafiri wa vyombo vya majini. Kusini mwa Maporomoko ya Ngonye, mto huo unapakana kwa muda mfupi na Ukanda wa Caprivi wa Namibia. Chini ya makutano kati ya Mto Cuando na Zambezi, mto unajipinda ukielekea takriban mashariki kabisa. Hapa, mto huo ni mpana, una kina kifupi na utiririka taratibu, lakini unapoendelea kutiririka kuelekea mashariki kukabili ukingo wa uwanda wa juu mkubwa wa kati wa Afrika, unafikia ufa mkubwa ambapo Maporomoko ya Victoria yanaporomoka.
Zambezi ya Kati
[hariri | hariri chanzo]Maporomoko ya Victoria yanachukuliwa kuwa mpaka kati ya upande wa juu na wa kati wa Mto Zambezi. Chini ya maporomoko hayo, mto unaendelea kutiririka moja kwa moja kuelekea mashariki kwa takriban kilomita 200 (maili 120), ukipenya katikati ya kuta zilizosimama wima za miamba ya mgando zenye umbali wa mita 20 hadi 60 (futi 66 hadi 197) kutoka ukuta mmoja hadi mwingine, zikiwa ndani ya vilima vyenye urefu wa mita 200 hadi 250 (futi 660 hadi 820). Mto huo hutiririka kwa kasi kubwa kupitia Bonde la Batoka, huku mkondo wake ukiwa unakatizwa mara kwa mara na miamba ya chini ya maji. Eneo hili limeelezwa[12] kuwa moja ya maeneo ya kusisimua zaidi duniani kwa safari za boti kwenye maji yanayovurugika, likiwa ni changamoto kubwa sana kwa waendesha mitumbwi ya kisasa ya 'kayak' na boti za raba za 'raft'. Ng'ambo ya bonde hilo kuna mfululizo wa maporomoko madogo ya maji yanayoishia kilomita 240 (maili 150) chini ya Maporomoko ya Victoria. Katika umbali huu, mto unashuka kwa mita 250 (futi 820).
Katika hatua hii, mto unaingia katika Ziwa Kariba, lililoundwa mwaka 1959 kufuatia kukamilika kwa Bwawa la Kariba. Ziwa hili ni moja ya maziwa makubwa zaidi yaliyotengenezwa na binadamu duniani, na mitambo ya kuzalisha umeme wa maji kwenye bwawa hilo inatoa umeme kwa sehemu kubwa ya Zambia na Zimbabwe.
Mito ya Luangwa na Kafue ndiyo matawi mawili makubwa zaidi ya mkono wa kushoto ya Mto Zambezi. Mto Kafue unaungana na mto mkuu katika mkondo wa maji uliotulia na wenye kina kirefu, wenye upana wa takriban mita 180 (futi 590). Kuanzia hapa, kona ya kuelekea kaskazini wa Mto Zambezi unazuiwa, na mkondo unaendelea moja kwa moja kuelekea mashariki. Katika makutano ya Mto Luangwa (15°37'S), mto huo unaingia nchini Msumbiji.[13]
Upande wa kati wa Mto Zambezi unaishia pale mto unapoingia katika Ziwa Cahora Bassa, ambalo hapo awali lilikuwa eneo lenye maporomoko hatari ya maji yaliyojulikana kama Kebrabassa; ziwa hili liliundwa mwaka 1974 kufuatia ujenzi wa Bwawa la Cahora Bassa.
Zambezi ya Chini
[hariri | hariri chanzo]Urefu wa kilomita 650 (maili 400) wa upande wa chini wa Mto Zambezi kutoka Cahora Bassa hadi Bahari ya Hindi unapitika kwa vyombo vya majini, ingawa mto huo una kina kifupi katika maeneo mengi wakati wa kiangazi. Hali hii ya kuwa na kina kifupi inatokana na mto huo kuingia kwenye bonde pana na kuenea katika eneo kubwa. Ni katika sehemu moja tu, kwenye Bonde la Lupata, umbali wa kilomita 320 (maili 200) kutoka kinywa chake, ambapo mto huo umebanwa katikati ya vilima virefu. Hapa, una upana wa karibu mita 200 (futi 660) tu. Katika maeneo mengine, una upana wa kilomita 5 hadi 8 (maili 3 hadi 5), ukitiririka taratibu kupitia mikondo mingi. Kingo za mto huo ni ya mchanga, na kingo zake ni za chini na zimezungukwa na matete. Hata hivyo, katika baadhi ya maeneo, na hasa wakati wa majira ya masika, mikondo hiyo huungana na kuwa mto mmoja mpana unaotiririka kwa kasi kubwa.
Takriban kilomita 160 (maili 99) kutoka baharini, Mto Zambezi unapokea maji yanayotoka Ziwa Malawi kupitia Mto Shire. Unapokaribia Bahari ya Hindi, mto huo unajigawa na kutengeneza delta. Kila moja ya mifereji mikuu ya mto inayojigawa—Kongone, Luabo, na Timbwe—imezuiliwa na ukingo wa mchanga. Tawi lililopo upande wa kaskazini zaidi, linaloitwa kinywa cha Chinde, lina kina cha chini kabisa wakati wa maji kupwa cha mita 2 (futi 6 na inchi 7) kwenye lango la kuingilia na mita 4 (futi 13) ukienda ndani zaidi, na hili ndilo tawi linalotumiwa kwa usafiri wa vyombo vya majini. Takriban kilomita 100 (maili 62) mbele zaidi kuelekea kaskazini kuna mto unaoitwa Quelimane, ukipewa jina la mji uliopo kwenye kinywa chake. Mkondo huu wa maji, ambao unajaa tabaka la mchanga na matope, unapokea maji ya ziada yanayofurika kutoka Zambezi wakati wa majira ya masika.[14]
Delta
[hariri | hariri chanzo]Delta ya Zambezi leo hii ina upana wa takriban nusu ya ule uliokuwepo kabla ya ujenzi wa mabwawa ya Kariba na Cahora Bassa kudhibiti mabadiliko ya msimu ya kasi ya utiririkaji wa mto huo. Kabla ya mabwawa hayo kujengwa, mafuriko ya msimu ya Zambezi yalikuwa na athari tofauti kabisa kwenye mifumo ya ikolojia ya delta ikilinganishwa na leo, kwani yalileta maji baridi yenye virutubisho vingi kuelekea kwenye ardhi oevu ya pwani ya Bahari ya Hindi. Upande wa chini wa Zambezi ulikuwa ukipata ongezeko dogo la ghafla la maji ya mafuriko mwanzoni mwa majira ya kiangazi wakati mvua katika eneo la bonde la Gwembe na kaskazini-mashariki mwa Zimbabwe ilipotiririka kwa kasi, wakati mvua kutoka upande wa juu wa Zambezi, Kafue, na mabonde ya Ziwa Malawi, pamoja na Luangwa kwa kiasi kidogo, zikiwa bado zimezuiliwa na mabwawa pamoja na nyanda za mafuriko.
Kutiririka kwa mifumo hii huchangia katika mafuriko makubwa zaidi mnamo mwezi Machi au Aprili, kukiwa na wastani wa kiwango cha juu cha mwezi kwa Aprili wa mita za ujazo 6,700 (futi za ujazo 240,000) kwa sekunde katika eneo la delta. Rekodi ya mafuriko makubwa zaidi ilikuwa kubwa zaidi ya mara tatu ya kiwango hicho, ambapo mita za ujazo 22,500 (futi za ujazo 790,000) kwa sekunde zilirekodiwa mnamo mwaka 1958. Kinyume chake, kiasi cha maji yaliyotiririka mwishoni mwa majira ya kiangazi kilikuwa na wastani wa mita za ujazo 500 (futi za ujazo 18,000) pekee kwa sekunde.
Katika miaka ya 1960 na 1970, ujenzi wa mabwawa ulibadilisha kabisa mfumo huo. Upande wa chini wa mto, wastani wa kiwango cha chini hadi cha juu cha mwezi ulikuwa mita za ujazo 500 hadi 6,000 (futi za ujazo 18,000 hadi 212,000) kwa sekunde; sasa hivi ni mita za ujazo 1,000 hadi 3,900 (futi za ujazo 35,000 hadi 138,000) kwa sekunde. Hasa mafuriko ya kiwango cha kati, ya aina ile ambayo ikolojia ya upande wa chini wa Zambezi ilikuwa imeafikiana nayo, yanatokea kwa uchache zaidi na yanachukua muda mfupi zaidi. Kama ilivyo kwa athari mbaya za Bwawa la Itezhi-Tezhi kwenye Nyanda za Kafue, jambo hili lina athari hizi zifuatazo:
- Mifumo ya ulishaji na uzalishaji wa samaki, ndege, na wanyamapori wengine ilivurugika.
- Zinabaki nyanda za nyasi chache zaidi baada ya mafuriko kwa ajili ya malisho ya wanyamapori na ng'ombe.
- Mifumo ya jadi ya kilimo na uvuvi ilivurugika.[15]
Ekolojia
[hariri | hariri chanzo]
Mifumo ya ja Delta ya Zambezi ina maeneo makubwa ya nyanda za nyasi zinazofurika kwa msimu na zile zinazofurika kudumu, savana, na misitu ya mabwawa. Pamoja na nyanda za mafuriko za Mito ya Buzi, Pungwe, na Save, nyanda hizi za mafuriko za Zambezi zinaunda eneo la ikolojia la savana ya pwani inayofurika ya Zambezi nchini Msumbiji, chini ya Mfuko wa Wanyamapori Duniani (WWF). Savana hizo zinazofurika zipo karibu na pwani ya Bahari ya Hindi. Misitu ya mikoko inazunguka pembezoni mwa ukanda wa pwani wa delta hiyo.

Ingawa mabwawa hayo yamedhibiti kiasi fulani cha mafuriko ya kila mwaka ya upande wa chini wa Mto Zambezi na kusababisha eneo la nyanda za mafuriko kupungua sana, hayajaondoa mafuriko kabisa. Hayawezi kudhibiti mafuriko makubwa kupita kiasi, na yamefanya tu mafuriko ya kiwango cha kati kutokea kwa uchache zaidi. Mvua kubwa katika upande wa chini wa Zambezi inapoungana na mtiririko mkubwa wa maji kutoka juu ya mto, mafuriko makubwa bado hutokea, na ardhi oevu bado inabaki kuwa makazi muhimu ya viumbe. Hata hivyo, kupungua kwa ardhi hiyo oevu kulisababisha ujangili na uwindaji usiodhibitiwa wa wanyama kama vile nyati na kulungu wakati wa Vita vya wenyewe vya Msumbiji.
Ingawa eneo hili limepungua idadi ya mamalia wakubwa, bado ni makazi ya baadhi yao, wakiwemo kulungu na pofu wanaohama. Wanyama wanaokula nyama wanaopatikana hapa ni pamoja na simba (Panthera leo), chui (Panthera pardus), duma (Acinonyx jubatus), fisi madoa (Crocuta crocuta), na bweha-milia (Canis adustus). Nyanda hizi za mafuriko ni maficho salama kwa ajili ya ndege wa majini wanaohama, wakiwemo bata-buzi mkia-mshale (pintails), bata-buzi mabawa-buluu (garganey), korongo dondola (Anastomus lamelligerus), korongo mdomo-wazi (Ephippiorhynchus senegalensis), korongo-nyani (Bugeranus carunculatus), na mtondo mweupe (Pelecanus onocrotalus).[16]
Wanyama watambaao ni pamoja na mamba wa Nile (Crocodylus niloticus), kenge wa Nile (Varanus niloticus), chatu wa Afrika (Python sebae), nyoka-nyoo wa Pungwe (Leptotyphlops pungwensis) ambaye anapatikana katika eneo hilo tu, na aina nyingine tatu za nyoka ambao wanakaribia kupatikana katika eneo hilo pekee: nyoka wa majini wa nyanda za mafuriko (Lycodonomorphus whytei obscuriventris), nyoka-mbwa kibete (Lycophidion nanus), na kipile wa marika/mabwawa (Proatheris).[16]
Aina kadhaa za vipepeo zinapatikana katika eneo hilo tu.



Hali ya hewa
[hariri | hariri chanzo]Upande wa kaskazini wa bonde la Zambezi una wastani wa mvua wa milimita 1100 hadi 1400 kwa mwaka, kiwango ambacho hupungua kuelekea kusini na kufikia takriban nusu ya idadi hiyo upande wa kusini-magharibi. Mvua hiyo hunyesha katika msimu wa mvua wa kiangazi unaodumu kwa miezi 4 hadi 6, wakati Ukanda wa Mkutaniko wa Hali ya Hewa wa Kitropiki unaposogea juu ya bonde hilo kutokea kaskazini kati ya Oktoba na Machi.[17] Viwango vya uvukizaji wa maji viko juu (milimita 1600 hadi 2300), na maji mengi hupotea kwa njia hii katika mabwawa na nyanda za mafuriko, hasa upande wa kusini-magharibi wa bonde hilo.[18]
Historia ya Jiolojia
[hariri | hariri chanzo]
Hadi kufikia mwishoni mwa kipindi cha Pliocene au Pleistocene (zaidi ya miaka milioni mbili iliyopita), upande wa juu wa Mto Zambezi ulitiririka kuelekea kusini kupitia eneo ambalo sasa hivi ni Bonde la Makgadikgadi hadi kwenye Mto Limpopo. Mabadiliko hayo ya mkondo wa mto ni matokeo ya misongezo ya kijiolojia ya kusaidiana kimaumbile ambayo iliinua uso wa ardhi kwenye eneo ambalo leo hii ni mgawanyaji wa maji kati ya mito hiyo miwili.
Wakati huo huo, umbali wa kilomita 1,000 (maili 620) kuelekea mashariki, kijito cha magharibi cha Mto Shire—katika upanuzi wa kusini wa Bonde la Ufa la Afrika Mashariki linalopita nchini Malawi—lilisababisha mmomonyoko uliotengeneza bonde lenye kina kirefu kwenye ukingo wake wa magharibi. Kwa kasi ya polepole, upande wa kati wa Mto Zambezi ulianza kumomonyoa na kurudisha nyuma sakafu ya mto wake kuelekea magharibi, ukisaidiwa na grabeni (mabonde ya ufa) zilizokuwa zikitengenezwa kwenye mkondo wake katika mhimili wa mashariki-magharibi. Ulivyofanya hivyo, uliichepua na kuimiliki mito kadhaa inayotiririka kuelekea kusini kama vile Luangwa na Kafue.

Hatimaye, ziwa kubwa lililokuwa limezuiliwa huko Makgadikgadi (au kijito chake) liliwahiwa na kuchepushwa na upande wa kati wa Mto Zambezi uliokuwa ukimomonyoka kurudi nyuma kuelekea lilipo, na hivyo likamwaga maji yake kuelekea mashariki. Upande wa juu wa Mto Zambezi nao ulichepushwa pia. Upande wa kati wa Mto Zambezi ulikuwa chini kwa takriban mita 300 (futi 980) ikilinganishwa na upande wa juu wa mto huo, na hivyo maporomoko makubwa ya maji yakatengenezeka kwenye ukingo wa uwanda wa juu wa miamba ya volkano ambapo mto wa juu unatiririkia. Haya ndiyo yalikuwa Maporomoko ya kwanza ya Victoria, mahali fulani chini ya Bonde la Batoka karibu na eneo ambalo sasa hivi lipo Ziwa Kariba.
Historia
[hariri | hariri chanzo]Uvumbuzi
[hariri | hariri chanzo]Ukanda wa Zambezi ulijulikana na wanajiografia wa zamani za kati kama Dola ya Monomotapa, na mkondo wa mto huo, pamoja na nafasi yalipo maziwa Ngami na Nyasa, vilichorwa kwa usahihi kwa ujumla katika ramani za mapema. Huenda ramani hizi zilitengenezwa kutokana na taarifa zilizotolewa na Waarabu.
Mzungu wa kwanza kutembelea sehemu za ndani za Mto Zambezi alikuwa degredado (msitiriwa/mfungwa wa kigeni) wa Kireno, António Fernandes, mnamo mwaka 1511 na tena mwaka 1513, akiwa na lengo la kutoa taarifa kuhusu hali na shughuli za kibiashara za maeneo ya ndani ya Afrika ya Kati. Taarifa ya mwisho ya uvumbuzi huo ilionyesha umuhimu wa bandari za upande wa juu wa Zambezi katika mfumo wa biashara wa wenyeji, hususan katika biashara ya dhahabu ya Afrika Mashariki.
Uvumbuzi wa kwanza kurekodiwa wa upande wa juu wa Mto Zambezi ulifanywa na David Livingstone katika safari yake ya uvumbuzi kutokea Bechuanaland kati ya mwaka 1851 na 1853. Miaka miwili au mitatu baadaye, alishuka kufuata mkondo wa Mto Zambezi hadi mdomoni mwake na katika safari hiyo aligundua Maporomoko ya Victoria. Katika kipindi cha mwaka 1858–1860, akiwa ameambatana na John Kirk, Livingstone alipanda mto huo kupitia mdomo wa Kongone hadi kufikia kwenye maporomoko hayo, na pia alifuatilia mkondo wa tawimto lake la Shire na kufika Ziwa Malawi.

Kwa miaka 35 iliyofuata, uvumbuzi mdogo sana ulifanyika kwenye mto huo. Mvumbuzi wa Kireno, Serpa Pinto, alichunguza baadhi ya mabonde ya magharibi ya mto huo na kufanya vipimo vya Maporomoko ya Victoria mnamo mwaka 1878. Mnamo mwaka 1884, mmishonari mzaliwa wa Scotland wa dhehebu la Plymouth Brethren, Frederick Stanley Arnot, alisafiri kupitia eneo lililoinuka la ardhi kati ya vyanzo vya maji (watersheds) vya mito ya Zambezi na Kongo na kugundua chanzo cha Mto Zambezi. Aliona kuwa Kilima cha Kalene kilichopo karibu—ambacho kiko juu na kina hali ya hewa ya baridi—kilikuwa eneo linalofaa hasa kwa ajili ya kituo cha umishonari. Arnot aliambatana na mfanyabiashara na afisa wa jeshi wa Kireno, António da Silva Porto.
Mnamo mwaka 1889, mfereji wa Chinde uliopo upande wa kaskazini wa midomo mikuu ya mto huo uligundulika. Misafara miwili ya uvumbuzi iliyoongozwa na Meja A. St Hill Gibbons kuanzia mwaka 1895 hadi 1896 na kuanzia 1898 hadi 1900 iliendeleza kazi ya uvumbuzi iliyoanzishwa na Livingstone katika bonde la juu na mkondo wa kati wa mto huo.
Matawimto
[hariri | hariri chanzo]Miji muhimu mtoni
[hariri | hariri chanzo]- Mongu
- Lukulu
- Katima Mulilo (Namibia), Sesheke (Zambia)
- Livingstone (Zambia), Victoria Falls (mji) (Zimbabwe)
- Kariba
- Songo
- Tete
Wanyamapori
[hariri | hariri chanzo]
Mto huo unahimili idadi kubwa ya wanyama wengi. Viboko wanapatikana kwa wingi katika maeneo mengi yenye mtiririko mtulivu wa mto huo, pamoja na mamba wa Nile. Kenge wanapatikana katika maeneo mengi. Ndege pia wako kwa wingi, kukiwa na aina za ndege kama vile kozi, mtondo/mwari, kulastara, nembe, na tai-fisi wanaopatikana kwa idadi kubwa. Misitu ya kando ya mto pia inahimili wanyama wengi wakubwa, kama vile nyati, pundamilia, twiga, na tembo.[19]

Mto Zambezi pia unahimili mamia ya aina za samaki, ambapo baadhi yao wanapatikana katika mto huo tu. Aina muhimu ni pamoja na rasi/perege, ambao huvuliwa kwa wingi sana kwa ajili ya chakula, pamoja na kambale, kacha, mninga, na aina nyingine kubwa za samaki. Papa-fahali wakati mwingine hujulikana kama 'papa wa Zambezi' kwa jina la mto huo, asichanganywe na jamii ya papa wa maji baridi wa Glyphis ambao pia wanaishi katika mto huo.
Tazama pia
[hariri | hariri chanzo]Marejeo
[hariri | hariri chanzo]- ↑ https://web.archive.org/web/20081217180850/http://files.gorongosa.net/filestore/348-patterns_hydrological_change_zambezi_delta.pdf
- ↑ "Réseau International des Organismes de Bassin". RIOB (kwa Kifaransa). Iliwekwa mnamo 2026-06-24.
- ↑ https://www.britannica.com/place/Zambezi-River
- ↑ "Zambezi River Facts and Information". www.victoriafalls-guide.net (kwa Kiingereza). Iliwekwa mnamo 2026-06-24.
- ↑ "Chavuma Falls | waterfall, Zambia | Britannica", Encyclopedia Britannica (kwa Kiingereza), iliwekwa mnamo 2026-06-24
- ↑ "Ngonye Falls". Zambia Tourism (kwa American English). Iliwekwa mnamo 2026-06-24.
- ↑ Pasanisi, Francesco; Tebano, Carlo; Zarlenga, Francesco (2016-02-25). "A Survey near Tambara along the Lower Zambezi River". Environments (kwa Kiingereza). 3 (1). doi:10.3390/environment. ISSN 2076-3298. Ilihifadhiwa kwenye nyaraka kutoka chanzo mnamo 2025-11-27. Iliwekwa mnamo 2026-06-24.
{{cite journal}}: CS1 maint: unflagged free DOI (link) - ↑ https://web.archive.org/web/20150904101922/http://www.muvitv.com/dilapidated-zambezi-source-site-worry-ikelenge-dc/
- ↑ https://web.archive.org/web/20150904101922/http://www.birdlife.org/datazone/sitefactsheet.php?id=7178
- ↑ Geology Page (2014-11-25). "Zambezi River". Geology Page (kwa American English). Iliwekwa mnamo 2026-06-24.
- ↑ "Zambezi River Facts and Information". www.victoriafalls-guide.net (kwa Kiingereza). Iliwekwa mnamo 2026-06-24.
- ↑ Sean Edington (2022-05-16). "Is rafting on the Zambezi River below The Victoria Falls Dangerous?". Safpar (kwa American English). Iliwekwa mnamo 2026-06-24.
- ↑ Van Valkenburgh, Blaire; White, Paula A. (2021-04-20). "Naturally-occurring tooth wear, tooth fracture, and cranial injuries in large carnivores from Zambia". PeerJ (kwa Kiingereza). 9: e11313. doi:10.7717/peerj.11313. ISSN 2167-8359. Ilihifadhiwa kwenye nyaraka kutoka chanzo mnamo 2025-11-19. Iliwekwa mnamo 2026-06-24.
{{cite journal}}: CS1 maint: unflagged free DOI (link) - ↑ "Zambezi - Encyclopedia". theodora.com (kwa Kiingereza). Iliwekwa mnamo 2026-06-24.
- ↑ Knifton, Dulcie (2004-07). Revise AS Level Geography for Edexcel Specification B (kwa Kiingereza). Heinemann. ISBN 978-0-435-10154-1.
{{cite book}}: Check date values in:|date=(help) - 1 2 "Zambezian coastal flooded savanna | Ecoregions | WWF". ecoregions.worldwildlife.org. Iliwekwa mnamo 2026-06-24.
- ↑ Jessica (2024-03-03). "Canoeing on the Zambezi River". The Travel Vibes (kwa American English). Iliwekwa mnamo 2026-06-24.
- ↑ https://gorongosa.org/research/research_documents/Patterns_Hydrological_Change_Zambezi_Delta.pdf[dead link]
- ↑ "Zambezi River | Physical Features | Britannica", Encyclopedia Britannica (kwa Kiingereza), iliwekwa mnamo 2026-06-24
Viungo vya nje
[hariri | hariri chanzo]- Watersheds of Africa: A20 Zambezi Ilihifadhiwa 12 Machi 2007 kwenye Wayback Machine.
| Makala hii kuhusu maeneo ya Afrika bado ni mbegu. Je unajua kitu kuhusu Zambezi (mto) kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni? Labda unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa? Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari. |